bayyinaat

Published time: 15 ,October ,2017      18:49:40
"Mwenye kufunga ndoa amekamilisha nusu ya dini yake, basi na amche Allah katika nusu iliyobakia." Au hadithi isemayo: "Miongoni mwa nyakati za kushuka rehma za Mwenyezi Mungu ni wakati wa...........
News ID: 116

Kwa kuzingatia kwamba, familia ina nafasi muhimu katika saada na kutengemaa au nakama, ihlaki na kuharibika watu katika kila jamii, Uislamu umetilia mkazo maalumu juu ya suala la ndoa na kujenga familia, na ukaweka vigezo vya tabia na maadili katika suala zima la kuchagua mke. Ndoa yenye saada na mafanikio ni ile ambayo misingi yake imesimama kwa ajili ya kuunda familia salama, imara na yenye nishati, uchangamfu na bashasha. Kwa hakika mwanadamu ni majumuu   yenye vipaji tele na uwezo tayarifu na hivyo ndoa inaweza kuandaa mazingira mwafaka kwa ajili ya kustawi na kuchanua vipaji vilivyojificha katika ujudi na uwepo wa mwanadamu huyu na dafina iliyoko katika kila ujudi wa ndani wa mtu. Mapenzi, kudhamini hawaiji za maisha, usimamizi wa familia, mamlaka, kujitosheleza, kupigania ukamilifu, kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu na kuwalea watu wema na wastahiki ni mambo ambayo yanawezekana kupatikana kwa kuweko ndoa. Miongoni mwa nukta muhimu katika maktaba ya malezi ya Mtume SAW, masahaba wema na dhuria wake (watu wa nyumba yake tukufu yaani Ahlul-Beit), ni mtazamo wao wa kimaanawi kuhusiana na suala la ndoa na upande wa utukufu wake. Ibara tunazozishuhudia katika hadithi zinathibitisha hili kwa njia tofauti. Miongoni mwa hadithi hizo ni ile iliyopokelewa kutoka kwa Bwana Mtume SAW akisema:  

 من تزوج فقد احرز نصف دينه فليتق الله في النصف الباقي


"Mwenye kufunga ndoa amekamilisha nusu ya dini yake, basi na amche Allah katika nusu iliyobakia." Au hadithi isemayo:

"Miongoni mwa nyakati za kushuka rehma za Mwenyezi Mungu ni wakati wa shughuli ya akidi, nikaha na kufunga ndoa."

Vile vile kuna hadithi nyingi ambazo zinaonesha kuwa, akthari ya miamala ya kifamilia inahesabiwa kuwa sawa na kufanya ibada. Mtume SAW amenukuliwa akisema kwamba:

"Mwanaume anayefanya bidii kwa ajili ya familia yake, ni sawa na mujahidi katika njia ya Mwenyezi Mungu."

Katika hadithi nyingine Mtume SAW amesema:

جهاد المرأه حسن التبعّل

"Jihadi ya mwanamke ni kuwa na mwenendo mwema kwa mume."

Kwa hakika ibara zote hizi zinaonesha jinsi Uislamu unavyoshajiisha juu ya suala la ndoa. Vile vile kunajitokeza uhakika huu kwamba, masuala ya maisha ya dunia yanaweza kuwa njia ya kuelekea katika ukamilifu wa kimaanawi na kiakhera. Miongoni mwa athari za kisaikolojia za ndoa, ni kuathiriana pakubwa mume na mke. Kila mmoja yaani mke na mume huathirika pakubwa na miamala, fikra na hata mtazamo wa mwenzake. Ni kwa kuzingatia uhakika huo, ndio maana maktaba ya kimalezi ya Mtume SAW, masahaba wema na dhuria wake ikakakoteza na kutilia mkazo juu ya kuzingatia suala la kuchagua mume au mke kabla ya kuoa au kuolewa na kuzingatia zaidi suala la thamani za kiakhlaqi na kimaadili.

Sababu ya jamii kuporomoka kimaadili katika ulimwengu wa Magharibi?

Hii leo mmonyoko uliokithiri wa kimaadili katika jamii za Kimagharibi chimbuko lake ni wanajamii kuweka kando mafundisho sahihi ya dini hasa kuhusiana na suala la ndoa. Si hivyo tu, Wamagharibi wamechupa mipaka na kuanza kutambulisha ndoa ambazo zinakinzana kabisa hata na maumbile ya mwanadamu. Tunashuhudia hii leo katika ulimwengu wa Magharibi kukieneza ndoa za watu wa jinsia moja, yaani ndoa baina ya mwanaume na mwanaume (usenge na ushoga) au baina ya mwanamke na mwanamke (usagaji), kitendo ambacho kimsingi sio ndoa na wala haifai kuita mafungamano hayo kuwa ni ndoa, bali ni uchafu ambao jina lake hasa ni usenge, liwati na usagaji. Nukta ya kutilia maanani hapa ni kwamba, dini zote na madhehebu zote zinavitambua vitendo cha usenge, ushoga, liwati na usagaji kuwa ni dhambi kubwa na kinyume kabisa na maumbile ya mwanadamu na zinawaonya wanadamu kujihusisha na vitendo hivyo.

Itaendelea…

Na Salum Bendera

LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: