bayyinaat

Published time: 15 ,October ,2017      18:55:28
Tab'an, hii leo ulimwengu wa Magharibi unakabiliwa na tatizo jingine nalo ni maisha ya kuweko mzazi mmoja kila familia. Yaani baadhi ya familia zina baba tu au mama tu na hivyo kupelekea .........
News ID: 117

Mpenzi msomaji, katika sehemu ya kwanza na ya pili za makala hii ya "Ndoa, Msingi wa Kujenga Familia", tuliashiria mambo kadhaa likiwemo suala la umuhimu wa ndoa katika jamii. Tulisema kuwa, ndoa ni jiwe la kwanza la msingi la kujenga familia, na familia ni taasisi kuu ya jamii. Tulizungumzia japo kwa muhtasari pia jinsi dini za mbinguni zilivyoshajiisha na kulipa umuhimu suala la ndoa na kueleza kwamba, Uislamu ndio dini iliyoko mstari wa mbele katika hili ambapo umeweka sharia, misingi na hata vigezo vya kuoa. Kadhalika tulitupia jicho matatizo na chimbuko la kuporomoka jamii katika ulimwengu wa Magharibi na kuona jinsi suala la ndoa lilivyo na umuhimu katika kujenga, kulinda na kuimarisha familia.

Ifuatayo ni sehemu ya pili na ya mwisho ya Makala hii.

Matatizo ya ulimwengu wa Magharibi

Tab'an, hii leo ulimwengu wa Magharibi unakabiliwa na tatizo jingine nalo ni maisha ya kuweko mzazi mmoja kila familia. Yaani baadhi ya familia zina baba tu au mama tu na hivyo kupelekea kuweko hali ya kulegalega ndani ya familia hizo. Hii leo kuna nchi nyingi barani Ulaya ambapo asilimia 50 hadi 80 ya watoto wamezaliwa nje ya ndoa. Ufaransa na nchi za Scandinavia ni miongoni mwa nchi hizo. Katika kipindi cha maisha yao yote, watoto hawa huishi na mzazi mmoja au kutoishi na wazazi wao wote wawili kutokana na kulelewa katika vituo maalumu vya malezi ya watoto. Utafiti uliofanywa unaonyesha kuwa, watoto wanaozaliwa katika familia na kukulia humo huwa wazima zaidi kimwili, kiafya na kisaikolojia na wakiwa shuleni au sehemu za kazi huwa na mahusiano bora, huishi maisha marefu na ni wenye furaha na bashasha ikilinganishwa na watoto ambao wamezaliwa nje ya familia. Kwa hakika ndoa ambayo wanandoa wake wamechaguana kwa kuzingatia masuala ya kimaanawi na maadili mema huwaandalia uwanja wa ukamilifu na saada ya dunia na akhera. Mtume SAW alifanya juhudi kubwa kueneza utukufu wa ndoa baina ya watu. Ni kwa kuzingatia uhakika huo, ndio maana Bwana Mtume SAW amenukuliwa katika hadithi mashuhuri akisema: 

النكاح من سنتي فمن رغب عن سنتي فليس مني 

Ndoa ni katika sunna yangu na mwenye kutenda kinyume na sunna yangu si katika mimi." Au hadithi hii iliyonukuliwa kutoka kwa Imam Jafar Sadiq (AS) mmoja wa wajukuu wa Mtume SAW inayosema:

 رَکعَتانِ یُصَلّیهِما المتزوج افضل من سيعين ركعة يصليها اعزب 

"Rakaa mbili (anazoswali) za mwenye kuoa ni bora (zenye thamani kubwa) kuliko rakaa sabini za  kapera (mtu ambaye hajaoa.)"

 

Mtazamo wa Uislamu juu ya vigezo vya ndoa

Katika mtazamo wa Mtume SAW na dhuria wake wema ni kuwa, endapo mke na mume watakuwa na sifa tatu za elimu, ustadi na tabia njema wanaweza kuiongoza na kuisimamia nyumba na familia kwa njia bora kabisa. Katika familia kama hii, mwanaume atakuwa kiongozi laiki, mstahiki, mwenye hima na mpole. Atadhamini mahitaji ya familia yake kwa njia za halali. Kwa msingi huo atakuwa mume mwema na mwenye mapenzi kwa familia yake. Uongozi na usimamizi wake kwa familia yake hautakuwa na misingi ya kutaka kutawala na utumiaji mabavu. Atakuwa mwanaume mwenye kuihami na kulinda familia yake na atakuwa ni mwenye kufanya jitihada kwa ajili ya kutoa miongozo na himaya kwa familia yake na bila shaka atawashajiisha wanafamilia kuelekea upande wa masuala ya kimaanawi. Nafasi ya mwanamke pia katika familia ina umuhimu mkubwa mno.

Jukumu muhimu la mke ndani ya nyumba

Kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu, jukumu muhimu la mwanamke ndani ya nyumba baada ya kutekeleza taklifu za kidini ni kumkidhia mumewe haja za kindoa. Subira na ustahamilivu wa mwanamke na kuwa pamoja na mumewe katika dhiki na faraja, katika matatizo ya kijamii na kiuchumi na vile vile kutokuwa na matarajio yaliyo nje ya uwezo wa mumewe ni mambo ambayo yanaweza kuandaa uwanja mwafaka wa kuweko uhusiano mwema, mzuri na unaofaa baina ya mume na mke; uhusiano ambao bila shaka utaimarisha pendo lao na kuizatiti ndoa yao. Katika upande mwingine, mwanamke ni kituo cha huba na mapenzi katika familia na jukumu la kuwalea watoto wema, wastahiki na wenye imani liko katika mabega yake kabla ya mtu mwingine yeyote yule.

Wabillah Tawfiki,

Na Salum Bendera

 

LABEL:
non-publishable: 0
Under Review: 0
Published: 1
2639/02/19 - 18:02
|
Iran, Islamic Republic of
|
Anonymous
0
0
Mashallah. Makala imenivutia sana. Allah akulipeni
Administrator SHukran sana
karibu na endelea kutembelea mtandao wetu
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: