Kwa hakika jambo
la kusherehekea mazazi ya Mtukufu Mtume Muhammad (saww) ni katika mambo ambayo
Waislamu wa dunia nzima wamelizoea kuanzia tangu na tangu, n apia ni katika
mambo ambayo yamekuwa yakidumishwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja mpaka
kingine, mpaka kufikia hali y akwamba swala hili limekuwa ni lenye kuadhimishwa
kuanzia ngazi ya mijumuiko mikubwa mpaka kufikia sasa limekuwa likiazimishwa
hata kwa ngazi za familia fulani.
Lakini hii yote ni
kwa minajili tu ya kuonyesha kwamba huyu mtu wanayemuadhimisha si kwamba ni mtu
wa kawaida, n a hivyo katika upande huu Waislamu wanakuwa kama Umma nyinginezo
ambazo zimekuwa zikiadhimisha masiku muhimu yao matukufu ikiwa ni pamoja na
kutukuza zama hizo takatifu.
Hili kwa asili ni
jambo jema sana na linalofaa kutukuzwa na kila mmoja, ila kwa kuwa tunataka
kufikia katika hali njema zaidi basi ni wajibu wetu kuweza kuhamisha ada hii
kutoka katika hali ya kusherehekea tu na kuihamisha katika hali ya kujifunza
mambo muhimu kutoka katika maadhimisho haya, hii sio mada yangu kwa siku ya
leo, japokuwa imepita kutokana na hali ya maneno kuvuta maneno yanayofanana
nayo.
Tukirudi katika mada
ni kwamba pamoja na kwamba kuna kila dalili ya kuonyesha kwamba swala la
kusherehekea au kukumbuka mazazi ya Mtume (saww) ni jambo jema na lenye
kusifiwa na wala halina tatizo lolote lile, bado unakuta kuna baadhi ya watu
ambao wao kila kukicha wao ni wenye kutafuta sababu tu za kuweza kusimamisha
jambo hili, nasema hivi kwa sababu mpaka leo hii bado hawajapata la kusema na
wala hawatakuja kupata la kusema katika kusimamisha swala hili. Japokuwa
wenyewe wanajinadi ya kwamba wamepata msingi wa kusimamisha swala hili.
Ila kwa mujibu wa
maneno yao au kwa ibara sahihi ni kwamba kutokana na wataalamu kusoma maneno
yao wamekuja kugundua kwamba, jambo ambalo limepelekea wao kuamini kwamba wana
hoja thabiti ya kusimamisha swala hili ni kutokana na ufahamu wao usio sahihi
katika kuelewa na kuelezea maana sahihi ya neno "Bidaa” "Uzushi katika dini”.
Na kutoelewa kwao huku kumepelekea kuharamisha mambo mengi sana ambayo yana
misingi katika dini yetu, kwa kuishia tu kusema kwamba mambo hayo hayana dalili
mahususi inayo yahusu.
Na hapa ndugu msomaji
ndipo ambapo ningependa kuanzia mazungumzo yetu haya kuhusiana na kusherehekea
mazazi ya Mtume (saww), ambapo kwanza tutaangalia uhalali n ausahihi wake, kisha
kuja kujadili hizo rai za hao ambao wanaamini kwamba wamefanikiwa kwazo
kusimamisha swala hili kisheria.
Ila katika kubainisha
swala hili kuna baadhi ya mambo kwanza ningependa yawe kama utangulizi n a
ufunguo wa kuingia katika mada yetu kwa hivyo vipengele viwili. Napenda
itambulike kwamba:
1.
Matukio matukufu siku zote huwa yanafanya masiku yake
kuwa na utukufu pia.
Hapa namaanisha nini?, nataka kusema kwamba siku kama siku haiwezi kuwa na
utukufu fulani ikiwa hakuna jambo tukufu ambalo limetokea ndani yake, angalia
mifano katika masiku kama Eid Fitr na Adh-ha, Usiku wa Lailatul Qadr, Masiku ya
mwezi wa Ramadhani, Siku ya kutumilizwa Bwana Mtume (saww), na matukio
mengineyo mengi mno, utakuta kwamba utukufu wa masiku haya unatokana na jambo
ambalo lipo ndani ya siku ile, na wala si asili ya siku yenyewe.
Mfano imepokelewa
katika riwaya za ubora wa siku ya Ijumaa kutoka katika Sahih Muslim kwamba
"......Mwenyezi Mungu alimuumba Adamu siku ya Ijumaa na pia kumpeleka Peponi
siku ya Ijumaa...”[1]
Au ukirejea katika
baraka za mwezi wa Ramadhani ni kwamba Mwenyezi Mungu mwenyewe amesema "......Mwezi
wa Ramadhani ambao ndani yake imeteremka Quran.....”[2].
Au kunako Usiku wa
Cheo na daraja "Lailatul Qadr”, unakuta Mwenyezi Mungu anasema "...Hakika sisi
tumeiteremsha katika usiku wa cheo, n
ani jambo gani litakalokujulisha ni upi huo usiku wa cheo?, usiku wa cheo ni
bora kuliko miezi Elfu moja.........”.[3]
Unakuta kwamba masiku
haya yote yamepata sifa hizo kutokana na uzito wa matukio ambayo yametukia
katika siku hizo.
Sasa tuje katika asili ya mada yetu n a
kujiuliza swali moja tu ambalo ni, ikiwa masiku hupata utukufu kutokana na
matukio yanaotukia ndani ya siku hiyo, kwanini siku ya kuzaliwa Mtume isiwe ni
katika mfumo huu pia?, yaani ikawa siku hii nayo inachukua utukufu kutokana na
tukio tukufu la kuzaliwa Bwana na mbora wa viumbe vyote, au kuna mwenye kukataa
kwamba kuzaliwa kwa Mtume Muhammad si katika matukio matakatifu?.
Itaendelea sehemu ya pili......