Fadhila zake
na Tabia zake njema
Miongoni mwa
fadhila kubwa za Imamu huyu ni kwamba kuna riwaya nyingi sana kutoka kwa Bwana
Mtume ambazo zimekuja katika kuelezea
hilo, miongoni mwa riwaya hizo ni:
·
Siku moja mmoja wa Masahaba anasema kwamba alimuona Mtume
amemuweka Imamu Hassan katika mabega yake
huku akisema ".....Kama unanipenda basi mpende na huyu”.
·
Pia imepokelewa kutoka Abuu Huraira kwamba amesema "....Hakuna
wakati ambao nimemuona Hassan nisiokwe na machozi, na hii ni kutokana na kwamba
siku moja nilimuona akimpandia Bwana Mtume kisha Mtume kuchukua mdomo wake na
kuuweka katika mdomo wa Hassan huku akisema "...Ewe Mwenyezi Mungu, mpende
mwenye kumpenda huyu, kwani mimi nampenda sana” mara tatu.[1]
Mbali na riwaya
hizo pia kuna riwaya nyingi mno kutoka kwa Mtume ambazo zote zinaashiria ubora
na fadhila za Imamu Hassan (as), kama zile riwaya zenye kusema ya kwamba Hassan
na Hussein ni viongozi wa vijana wa peponi, au riwaya zote zenye kuamrisha
kumpenda yeye kwani Mtume mwenyewe alikuwa akimpenda kijana huyu.
Mahusiano yake
na Mungu wake:
Kama tunavyojua ya
kwamba moja ya mambo ambayo yanafanya watu hawa waweze kuwa bora mbele ya Mwenyezi
Mungu, ni kutokana na mshikamano wao wa nguvu na muumba huyo. Basi hata tukija
kwa Imamu Hassan pia tunakuta kwamba hakuwa mbali na ada na mstari huo, kwani
inapokelewa kwamba Imamu Hassan alikuwa ni mwenye kuabudu zaidi katika zama
zake, mwenye kuipa dunia mgongo zaidi kuliko watu waote wa zama zake.
Tunaambiwa kwamba
alikuwa akitekeleza ibada yake ya Hijja
miaka yote kwa kutembea kwa miguu, na kuna baadhi ya riwaya zinasema kwamba
mbali na kutembea kwa miguu bado alikuwa akitembea peku. Alikuwa akikumbuka
kifo, kupita katika sirat, siku ya kukutana na Mungu hulia mpaka kufikia hatua
ya kuzimia.
Kifupi ni kwamba
katika maisha ya Ibada ya Imamu Hassan, tunaweza kupata masomo yafuatayo:
·
Ibada haina maana kwamba mwanadamu ajitenge kabisa na
wenzake, kwani pamoja na kwamba Imamu alikuwa yu karibu sana na Mwenyezi Mungu
bado tunakuta maisha yake ya kijamii yalikuwa ni yenye kuimarika katika kila nyanja.
·
Ibada si tu matendo maalumu ya Kidini kama vile Swala,
Funga na mengineyo. Bali kila tendo ambalo kulifanya kwake kunakuwa na kutafuta
radhi ya Muumba huhesabika ni ibada. Matendo kama kusaidia wengine, kushiriki
katika shughuli za kijamii, kuishi vizuri na watu na mengineyo, endapo
yatafanywa kwa nia ya kutafuta radhi za Mwenyezi mungu basi huingia katika
ibada pia, hivyo hakuna haja ya kukaa nyuma katika maswala hayo.
·
Ibada haina maana kwamba unakuwa umeepukana na sheria za
Muumba. Kwa maana ya kwamba kufanya kwako ibada kusikuweke katika hali ya kuona
kwamba tayari umeshamaliza kila kitu, na kwamba hakuna tena jukumu lolote
ambalo unatakiwa kulisimamia, bali mwanadamu pamoja na kufanya ibada zake, bado
anatakiwa kubakia katika hali ya shauku juu ya ibada zake, kwani hakuna
anayejua uhakika wa kukubaliwa au kukataliwa ibada zake.
Upole wake
Katika sifa za Imamu
Hassan ni upole, upole ambao kwao aliweza kuwavuta watu katika dini ya Mwenyezi
Mungu bila hata ya kutumia nguvu nyingi.
Inapokelewa kwamba
siku moja alikuja mzee kutokea mji wa Sham na kuanza kumtukana Imamu (as), Imamu
akamsikiliza mpaka alipomaliza na kumwambia "....Ewe Mzee wangu, najua kwamba
ni mgeni maeneo haya, na najua fika kwamba umeshaambiwa mabaya kuhusu sisi,
lakini laiti kama ungaliniomba msaada basi ningalikusaidia, na kama
ungaliniuliza njia basi ningalikuelekea, na kama ulikuwa unahitajia jambo basi
ningali kusaidia, na kama huna makazi basi tutakupatia, na kama muda utaamua
kuondoka na sisi na kuamua kuwa mgeni wetu mpaka siku ya kuondoka kwako basi
itakuwa ni vyema zaidi kwako, kwani tuna sehemu kubwa na mali za kutosha kwa
ajili ya kukirimu wageni”.
Yule mzee baada ya
kusikia maneno hayo akasema "....Naapa kwa Mwenyezi Mungu kwamba wewe ni
kiongozi wa Mungu katika uso wa dunia, na kwa hakika Mungu hujua ni sehemu gani
ya kuweka ujumbe wake, hakika wewe pamoja na baba yako mlikuwa ni watu ambao
nawachukia sana, lakini kuanzia sasa nyinyi ni viumbe ni wapendao kuliko wote
katika dunia..” Kisha akakusanya mizogo yake na kuelekea nyumbani kwa Imamu na
kubakia naye kwa siku kadhaa mpaka alipoondoka.[2]
Huruma kwa
wanyama:
Huruma kwa viumbe
hai ni moja ya ishara za utu na ukarimu wa mwanadamu, kwa maana katika maisha
yetu kuna viumbe vingine ambavyo tunashirikiana navyo na ambavyo vinahitaji
ushirikiano kutoka kwetu.
Huu ushirikiano
ndio ambao tunaukuta kwa Imamu Hassan (as), kwani inapokelewa kwamba siku moja
alikuwa anakula chakula na pembeni yake kukiwa na mbwa, na kila ambapo alikuwa
anakula tonge moja basi la pili yake alikuwa akimtupia mbwa yule. Sahaba mmoja
akapita na kumuuliza Imamu juu ya jambo lile, Imamu akasema ".....Naam, muache
ale, kwa maana ninaona haya kula chakula wakati ambao kuna kiumbe hai
kinaniangalia na mimi nisimpatie chakula kile..”
Miongoni mwa
nasaha za kutoka kwake:
Zifuatazo ni baadhi
za nasaha kutoka kwa Imamu Hassan (as) katika kuhakikisha kwamba wanadamu wanakuwa
katika mstari ulionyooka na hatimaye maisha yetu baada ya duniani yanakuwa pia
katika hali nzuri.
·
Anasema "....Ewe mwanadamu, hakika maisha yako yapo
katika hali ya kupotea tangu siku uliyotoka tumboni kwa mama yako, basi
jitahidi kufanya yenye faida kwako, kwani muumini siku zote hujiandaa kwa ajili
ya kesho, lakini kafiri huona maisha ni ya duniani tu...”.
·
Anasema ".....Kuosha mikono kabla ya chakula huondoa
ufukara, kama ambavyo kuosha baada ya chakula pia huondoa huzuni”.
·
Anasema ".....Uulizaji mzuri ni nusu ya jawabu”. Kwa maana
ya kwamba ili kupata jibu la swali lako basi unatakiwa uwe na njia nzuri za
kuuliza swali lile, maana uulizaji mbaya unaweza kupelekea kukosa jawabu au
kupata jawabu lisilo kamili.
Huyu ndiye Imamu
Hassan (as) kwa kifupi, kwani hakuna anayeweza kuandika kwa kiwango cha ubora
wa watu hawa.
Imeandikwa na Sh
Abdul Razaq Bilal.