bayyinaat

Published time: 11 ,November ,2018      19:11:39
Elimu: awali ya yote tutaanza kuelezea maana ya Elimu, ambapo kuna maana tofauti ziliolezwa kunako suala zima la kuitambulisha neno Elimu, nami nitajaribu kuashiria baadhi yake kama ifuatavyo:
News ID: 357

Maana ya Elimu na Dini:

Elimu: awali ya yote tutaanza kuelezea maana ya Elimu, ambapo kuna maana tofauti ziliolezwa kunako suala zima la kuitambulisha neno Elimu, nami nitajaribu kuashiria baadhi yake kama ifuatavyo:

1- Elimu ni kufahamu na kuelewa jambo, kitu au kadhia fulani. Ikimaanisha kuwa kufahamu kwa aina yeyote kunako jambo au kitu chochote inasadikiwa kuwa mtu mwenye ufahamu huo amepata elimu ya jambo hilo, katika maana hii ya Elimu inakusanya aina zote za Elimu kwa maana inashamili Elimu inayopatikana kwa kuingia darasani kama vile Elimu za Sayansi, Mitafizikia na zingine zinazohitaji kujifunza, halikadhalika Elimu isiohitaji kuingia darasani, kama vile kuhisi kuwa umepatwa na maradhi au maumivu, huzuni, furaha na mengine yanayo fanana na hayo, kwa maana linapotajwa neno furaha, huzuni, maumivu ya kichwa nk, mtu huzifahamu kinachokusudiwa hata bila ya kufunzwa. Pamoja ya kwamba maana hii ilioashiriwa ni maana ya neno Elimu katika vitabu na semi za Lugha.

Ama maana ya Elimu katika Istilahi mbalimbali nitaashiria maana kadhaa kama ifuatavyo:

2- Ni kufahamu na kuelewa jambo ambako kunakoendana na uhalisia, kwa maana kila kuelewa au kufahamu ambapo kunaendana na uhalisia na uhakika, ndio kutaabiriwa kuwa ni Elimu, ama kama itakuwa ni kufahamu ambako hakukuambatana na uhakika uhalisia wa jambo hilo, haitasihi kuitwa Elimu kwa mujibu wa maana hii, kwa mfano mtu akafahamu yakuwa fulani amefariki, itasadikiwa kuwa ni Elimu endapo itakuwa kweli yule mtu kwa uhakika amefariki kweli, ama kama itakuwa kinyume chake haitasadikiwa kuwa ni Elimu. Ambapo katika maana ya awali, ilikuwa ni suala la kufahamu pekee bila ya kuambatana na ukweli na uhalisia wake, kulihesabiwa kuwa ni katika Elimu.

3- Ni ufahamu unaofikiwa kwa mafunzo ukaendana na uhalisia na uhakika wa ufahamu huo, kwa maana hii imepunguza kushamili misdaki na mifano mingi iliyoshamili katika maana ya pili, kwani katika maana ya pili ilishamili Elimu inayopatikana kwa kujifunza kwa kuingia darasani na Elimu isiopatikana na mafunzo, ama katika maana hii ni Elimu inayopatikana na kwa kujifunza kama vile Elimu za Sayansi, Elimu ya dini, Falsafa na kadhalika, ama zisizokuwa hizo hutoka katika hisabu ya Elimu.

4- Ni Elimu inayopatikana kwa njia ya Sayansi, kwa maana Elimu inayofikiwa kinyume na mifumo wa Sayansi haitahisabiwa kuwa ni katika Elimu, hivyo katika maana hii aina nyingi za Elimu hukosa hadhi na kutoka katika mjumuiko wa Elimu, kama vile Elimu za Metafizikia, Falsafa, Mantiki na kuendelea, ambapo mjadala mkubwa unaoendelea kuhusu fungamano la dini na Elimu, ni kutokana na maana hii ya Elimu iliotambulishwa kuwa ni Elimu inayopatikana kwa njia ya Sayansi, ambazo zimepita hatua zote za kisayansi.

Hizi ni baadhi ya maana ya neno Elimu katika nyanja mbalimbali za kielimu Jawadi [1]

Ama ukiangalia kwa undani zaidi kunako suala hili utaona kwamba suala na jambo muhimu katika kusadiki kwa neno Elimu ni kuwepo uhalisia wa jambo hilo, hivyo basi haijalishi kuwa uhalisia huo utafikiwa kwa njia Sayansi au Mantiki na Falsafa halikadhalika njia ya Mitafizikia, maadamu kuna uhalisia wa jambo hilo, basi tunaweza tukatumia neno Elimu na kusiwe na tatizo lolote, kwani kiwango hicho hutabezwa kwa watu wenye akili.

Inshallah tumuombe mwenyezi Mungu alimu atupe tawfiki ya kuwa pamoja tena katika makala ijayo itakayoelezea maana ya dini na mengineyo.

Wasalamu alaykum warahmatullah.

Imeandikwa na Sh Bakari Ally Matenga.



[1] Fungamano la Elimu na Dini, Allamah Jawad Amuliy uk 43-80” .


maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: