bayyinaat

Published time: 06 ,March ,2017      00:02:45
Neno 'Adl' hasa limetungwa kuleta maana ya "kufanya vitu viwili sawa" na "kugawa sawasawa" kwa lengo la kutekeleza haki na wema. Vivyo hivyo kwa neno 'Insaaf' ambalo maana yake hasa ni "kugawa sehemu mbili". Wazo la kugawa sawasawa linaleta maana ya "usawa" au "uadilifu"........
News ID: 37

SEHEMU YA KWANZA

(1)   MAANA YA 'ADL'  (uadilifu)

Neno 'Adl' hasa limetungwa kuleta maana ya "kufanya vitu viwili sawa" na "kugawa sawasawa" kwa lengo la kutekeleza haki na wema. Vivyo hivyo kwa neno 'Insaaf' ambalo maana yake hasa ni "kugawa sehemu mbili". Wazo la kugawa sawasawa linaleta maana ya "usawa" au "uadilifu". Kwa hivyo, neno 'Adl' lina maana ya "Uadilifu", "Usawa", "haki", "kufanya mambo mema,' "unyofu", "kutopendelea" na "kutoonea". Kinyume chake ni 'Jawr' na "Dhulm'. 'Jawr' maana yake ni "kupendelea". "Kuonea" na "Ujeuri". 'Dhulm' maana yake ni "kuweka kitu mahala pasipohusika" kama vile, hakimu mwonevu katika hukumu yake anavyomnyima haki mwenye kuonewa na hivyo anaweka hukumu yake mahali pasipohusika, basi huitwa "Dhalimu" Kufuatana na madhehebu ya Shia Ithnaasharia, Uadilifu ni moja katika sifa muhimu kabisa za Mwenyezi Mungu. Kuwepo kwa Mwenyezi Mungu na Umoja wake huja chini ya mzizi wa kwanza wa dini, "Tawheed" na vimeelezwa katika kitabu chetu "Mungu wa Uislamu". Lakini Vitendo vya Mwenyezi Mungu huja katika huu Msingi wa Pili, yaani Uadilifu. Ilivyokuwa tofauti kati ya Waislamu juu ya Uadilifu wa Mwenyezi Mungu ni kubwa na ya namna nyingi basi ni lazima kuzisoma sura zifuatazo kwa makini. Kumbuka kwamba kila neno au fungu la maneno katika sura hizi lina maana na ikiwa msomaji atajaribu kulibadilisha neno lolote au fungu lolote la maneno, basi atajitia katika msongamano wa hitilafu na maneno yasiyohusika.

(2) MEMA NA MAOVU

 Tofauti kuu ya kwanza ni kuwa madhehebu ya Sunni wanaamini kwamba kitu chochote kwa dhati yake yenyewe si chema wala kiovu na kwamba kile Mungu anachotuamrisha kufanya kinakuwa chema, na kile Anachokataza kinakuwa kiovu. Kwa upande wa pili, madhehebu ya Ithnaasharia wanaamini kuwa, bila kujali maamrisho ya dini, kuna mema na maovu katika vitendo mbalimbali, hii ndiyo sababu kwamba Mwenyezi Mungu anatuamrisha kufanya kitendo hiki kwa sababu ni chema na Anatukataza kufanya kitendo kile kwa sababu ni kiovu.

(3) VITENDO VYA MWENYEZI MUNGU

 Mwenyezi Mungu hatendi makosa au maovu. Situmii kifungu hiki kwa maana ya "Mfalme hafanyi makosa", kwa sababu "Mfalme hafanyi makosa" maana yake hasa ni kwamba yeye hafanyi chochote isipokuwa hutia sahihi yaliyopasishwa na Bunge. Lakini "Mwenyezi Mungu hafanyi makosa" maana yake ni kwamba Yeye ni Hodari na Mwenye Nguvu, lakini hafanyi makosa. Yeyote anayefanya makosa au Dhulma, hufanya ama kwa sababu hajui kwamba kufanya hivyo ni makosa, (lakini Mwenyezi Mungu anajua kila kitu), au kwa sababu yeye huhitaji kitu ambacho hawezi kukipata ila kwa kufanya maovu, (lakini Mwenyezi Mungu si Mhitaji). Au kwa sababu amelazimishwa na mtu kufanya huo uovu. (Lakini Mwenyezi Mungu ni Mwenye Uwezo juu ya kila kitu na hakuna mtu ye yote awezaye kumlazimisha). Hivyo, haiwezekani kiakili kwa Mwenyezi Mungu kufanya dhulma au makosa yo yote.

 (4) KILA KITU KINA SABABU

Mwenyezi Mungu daima hatendi kitu bila ya shabaha, yaani bila ya sababu au makusudio. Vitendo vyake vyote vinatokana na busara na sababu ya kiujuzi, ingawaje hatuwezi kuzijua. Kwa upande wa pili, Sunni wanasema kwamba, hakuna maovu hasa katika kufanya bila shabaha, na ikiwa Mwenyezi Mungu anafanya chochote bila ya sababu, basi kufanya huko kwa Mwenyezi Mungu kutakifanya kitendo hicho kuwa chema.

Itaendelea....

LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: