News ID: 375
Taarifa ya mwishoni mwa kongamano la siku mbili lililofanyika mjini Islamabad, Pakistan kwa anuani ya "Rehma kwa Walimwengu" limetoa sisitizo juu ya ulazima wa Waislamu duniani kushikamana na Uislamu wa asili kwa mujibu wa mafundisho ya Bwana Mtume Muhammad SAWW.
Taarifa hiyo iliyotolewa jana imeeleza kuwa, ili kuweza kufuata njia ya Uislamu wa asili, inapasa Waislamu wajiepushe na mifarakano na badala yake kushikamana na sira ya Ahlul-Beit wa Mtume SAW.
Taarifa hiyo aidha imesisitiza kuwa Bwana Mtume Muhammad SAW alikuwa Mtume adhimu aliyekuwa akitilia mkazo sana kuheshimu dini za watu wengine na kuwataka Waislamu wajiepushe na ubaguzi wa aina yoyote ile, lakini kuna watu majahili wanaotumia kila njia ili kuharibu sura ya dini tukufu ya Uislamu.
Kongamano la Rehma kwa Walimwengu limebainisha kuwa kutusi matukufu ya kidini si kutumia uhuru wa maoni na kujieleza ila ni kosa na uhalifu mkubwa.
Wakati huohuo Rais Arif Alawi wa Pakistan, ambaye alihutubia hafla ya ufungaji wa kongamano hilo, amesema mafundisho ya Nabii Muhammad SAW, ambayo yanatilia mkazo udugu na usawa baina ya Waislamu,ndiyo dira ya kuongoza umma wa Kiislamu.
Kongamano la Rehma kwa Walimwengu lililoanza siku ya Jumatano na kukamilisha shughuli zake jana Alkhamisi katika mji mkuu wa Pakistan, Islamabad limefanyika kwa mnasaba wa Wiki ya Umoja likishirikisha maulamaa kutoka nchi mbalimbali waliojadili na kubadilishana mawazo kuhusu mafundisho ya Bwana Mtume SAW, sira na maisha yake pamoja na kuwepo mashauriano kati ya madhehebu za Kiislamu
maoni Viewers