bayyinaat

Published time: 06 ,March ,2017      14:49:10
Kwanini watu wengi wamekuwa wakiogopa kifo? Kuna sababu gani nyuma yake? Hapa ndipo tutaanzia makala hii ambayo inalenga kumuelimisha Mwislamu juu ya uhakika wa Kiyama au siku ya marejeo. Na hii ni kutokana na kwamba hakuna njia ambayo tunaweza kupita ili kufikia siku hiyo tofauti........
News ID: 40

Je kifo ni mwanzo au mwisho?

Kwanini watu wengi wamekuwa wakiogopa kifo? Kuna sababu gani nyuma yake? Hapa ndipo tutaanzia makala hii ambayo inalenga kumuelimisha Mwislamu juu ya uhakika wa Kiyama au siku ya marejeo. Na hii ni kutokana na kwamba hakuna njia ambayo tunaweza kupita ili kufikia siku hiyo tofauti na kifo au mauti, na kwakuwa siku zote kifo kimekuwa ni kitu ambacho kwa mwanadamu ni chenye kutisha mno, na wakati mwingine hata kumnyima uhuru na furaha ya kutenda majukumu yake muhimu kuelekea kwa mola wake, na si tu kwamba neno kifo au kifo chenyewe ndivyo humwogopesha mwanadamu bali tunakuta wakati mwingine mwanadamu huyu anakuwa ni hata mwenye kuogopa makaburi yanapokuwa katika hali yake ya kawaida, na ndipo wengine leo hii hujitahidi kuyafanya makaburi hayo kuwa mfano wa majumba ya kifahari ili tu angalau iweze kuwasahaulisha uhakika wa nyumba ile ya kila mmoja wetu. Je kuna nini katika hiki kifo mpaka kimekuwa ni kitu chenye kuogopesha na kutisha kiasi hiki?.

Lakini pia hebu tuangalie upande wa pili, upande ambao tunakuta kuna baadhi ya watu ambao hawakiangalii kifo kwa sura ambayo kinaangaliwa na watu tuliotoka kuwazungumzia hapo juu, hapa tunawakuta watu hawa wanakiangalia kifo kwa namna ya kukifurahia na hata kutamani kiwajie wakati wowote. Kwani tukirejea katika historia tunaambiwa kwamba kuna baadhi ya watu ambao walikuwa wakikesha kutafuta mambo ambayo yatawafanya siku zote wawe hai na vijana, wakati ambapo kuna ambao walikuwa siku zote wakitamani Jihadi ije ili wakapigane na waelekee kwa mola wao, nini siri na sababu ya kila kundi katika makundi haya?.

Kwanini tunaogopa kifo?

Kama tutakuwa ni wenye kufanya tafiti basi tutafikia katika natija ya kwamba hofu ya kifo inatokana na mambo makuu mawili:

1.     Kutafsiri kifo kwamba ndio mwisho wa kila kitu

Hii ikiwa na maana kwamba kawaida ya mwanadamu siku zote amekuwa ni mwenye kukimbia sana swala la kutokuwepo na kupenda mno swala la uwepo. Mwanadamu anapenda sana uwepo wa afya na hapendi hata siku moja afya ile isiwepo, na ndio maana anajitahidi kadri awezavyo ili tu asipate maradhi na abakie ni mwenye afya siku zote. Kama ambavyo mwanadamu huyu anakimbia sana giza ambalo humaanisha ukosekanaji wa nuru na mwangaza, na mifano mingi ambayo inaweza kuthibitisha jambo hili. Lakini jambo la kushangaza zaidi ni kwamba mwanadamu huyuhuyu anamkimbia hata ambaye jana alikuwa hai (maiti) hii yote ni kwanini, ni kwamba siku zote uwepo wa kitu unapenda kuambatana na uwepo mwenzake, yaani mwanadamu anaamini kwamba yeye yupo, kwa hivyo ni lazima pembeni yake kuwe na kitu ambacho kipo na si kitu ambacho kimepoteza uwepo. Sasa hapa ndipo tunapata jibu la kwanini mwanadamu anakuwa ni mwenye kuogopa kifo au hata maiti na makaburi pia, ni kwamba mwanadamu huyu ameweka katika akili yake kwamba kifo ni mwisho wa kila kitu kama ambavyo pia kifo ni kutokuwepo kwa kitu, na ndio maana kutokana na msingi wake wa kupenda kuwa na vitu ambavyo vipo katika uwepo, anatokea kuchukia kifo kwa sababu tu kifo si kitu ambacho kipo, bali ni mwisho wa kila kitu.

 

2.    Ukurasa mchafu

Hii ni sababu ya pili ambayo inasababisha wanadamu kuogopa kifo, kwamba kuna wakati unakuta mtu anakubali kwamba kifo siyo mwisho wa maisha au mwisho wa kila kitu, na kwamba kuna maisha baada ya kifo, lakini bado unakuta mtu huyu anaogopa kifo kile. Sababu ni kwamba mtu wa namna hii anakuwa hana matendo mazuri ambayo ameyatanguliza ili kesho atakapokwenda katika huo ulimwengu wa baada ya kifo yawe ni yenye kumwokoa, na ndipo unakuta mtu kama huyu pia anaogopa kifo pamoja na kwamba haamini kwamba ni mwisho wa kila kitu.

Na hii ndiyo hali ya kila mwovu hapa ulimwenguni, anatamani kwamba maisha haya yawe ndiyo maisha yake milele, kwani anajua kwamba endapo maisha haya yatakatika na kuanza maisha mengine baada ya haya, bila shaka atakuwa katika adhabu na masikitiko makubwa. Lakini kwa ambao ni wema hapa ulimwenguni tunakuta kwamba mambo ni kinyume kabisa, kwani hawa wanajua kuwa furaha ya kudumu inapatikana baada ya kifo, hivyo ndio maana kifo kwao kinakuwa ni chenye kusubiriwa muda wote tena kwa furaha.

Muhimu

     Kifo sio mwisho wa maisha ya mwanadamu, bali ni mwanzo wa maisha ya awamu ya pili ya mwanadamu huyo.

Tukutane wakati ujao katika mwendelezo wa makala hizi.

Sh Abdul Razaq Bilal.

maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: