bayyinaat

Published time: 08 ,October ,2017      10:16:18
Miongoni mwa fahari na fadhila kubwa ambazo Shia na Sunni wanakubaliana nazo kuhusu Imam Ali (a.s), na kauli hizi za Mtume alizosema kunako yeye.......
News ID: 107

Katika riwaya mbalimbali na historia zimebainisha kwa upana kunako fahari na ubora wa Ali (a.s), ambapo sisi hapa tutabainisha kadhaa katika fadhila zake mfano; Haki iko pamoja na Ali, Msaidizi na mwenye kumnusuru Mtume (s.a.w), Ali ni sababu ya Malaika kujifaharisha kwa kumjua, katika tukio la kuombeana laana (المباهلة) Ali alikuwa ni nafsi ya Mtume, na kadhalika, nasi tutajaribu kukuleteeni fakhari za Imam huyu mtukufu ambazo zimethibiti , pia tutathibitisha kwa mujibu wa Qur’ani na Riwaya inshaallah.

1.               MALAIKA WAJIFAKHARISHA KUMTAMBUA IMAM ALI (A.S)

Mtukufu Mtume (s.a.a.w) alimwambia Imam Ali (a.s): "Ee! Ali, mbinguni wako Malaika wanaosubiri kukutana na wewe, wanakumbushana fadhila zako, kwa kukutambua wewe wanajifaharisha na kukujua wewe wanajikurubisha mbele ya Mwenyezi Mungu. Idadi yao hakuna awajuaye ila Mwenyezi Mungu pekee, Ewe! Ali, hakuna mwenye nafasi bora kwa waliotangulia kuliko nafasi yako na hakuna atakayekuwa na nafasi bora kwa wanaokuja”.[1]

 

 

2.               HAKI IKO PAMOJA NA ALI (A.S)

Miongoni mwa fahari na fadhila kubwa ambazo Shia na Sunni wanakubaliana nazo kuhusu Imam Ali (a.s), na kauli hizi za Mtume alizosema kunako yeye:

Amesema Mjumbe wa Mwenyezi Mungu:

«علیٌّ مع الحقّ و الحقّ مع علیٍّ و لن یفترقا حتّی یردا علیّ الحوض یوم القیامة».

 "Ali yuko pamoja na haki na haki iko pamoja na Ali, na kamwe havitoachana hadi vinifikie kwenye Hodhi siku ya Kiama”.[2]

Na katika nukuu nyingine amesema:

«علیٌّ مَع الحقّ و الحقّ مع علیٍّ و الحقّ یَدورُ حَیثُما دارَ عَلیٌّ». 

"Ali yuko pamoja na haki na haki iko pamoja na Ali, inazunguka popote alipo Ali”. Kwa maana kwamba, Ali ni mpambanuzi halisi wa haki.[3]

3.               IMAM ALI (A.S); NI NAFSI YA MTUME (S.A.W)

Kwa mujibu wa Aya:

«فَمَنْ حَاجَّكَ فيهِ مِنْ بَعْدِ ما جاءَكَ مِنَ الْعِلْمِ فَقُلْ تَعالَوْا نَدْعُ أَبْناءَنا وَ أَبْناءَكُمْ وَ نِساءَنا وَ نِساءَكُمْ وَ أَنْفُسَنا وَ أَنْفُسَكُمْ ثُمَّ نَبْتَهِلْ فَنَجْعَلْ لَعْنَتَ اللَّهِ عَلَى الْكاذِبينَ».

"Watakao kuhoji katika haya baada ya kukufikilia ilimu hii waambie: Njooni tuwaite watoto wetu na watoto wenu, na wake zetu na wake zenu, na sisi wenyewe na nyinyi wenyewe, kisha tuombe kwa unyenyekevu tutake laana ya Mwenyezi Mungu iwashukie waongo”.[4]

Na ya kwanza ya surat at-tawbah:

«بَراءَةٌ مِنَ اللَّهِ وَ رَسُولِهِ إِلَى الَّذينَ عاهَدْتُمْ مِنَ الْمُشْرِكينَ».

"Huku ni kujitoa Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwenye jukumu la maagano na mlio ahidiana nao katika washirikina”.[5]

Ali katika aya ya kwanza ni nafsi ya Mtume, na kwa mujibu wa aya ya pili,[6] wafasiri wamesema kwamba; Mara ya kwanza Mtume (s.a.w) alimtuma khalifa wa kwanza kufikisha ujumbe huo, lakini Malaika kutoka kwa Mungu alikuja na kusema; Mwenyezi Mungu baada ya kukutolea salamu anasema; Mtume Mtu ambaye anatokana na wewe, wakati huo Mtume (s.a.w), akamtaka Amirul Muuminiin kukamilisha misheni ile.

4.               ALI (A.S) NI KHALIFA NA WAZIRI WA MTUME (S.A.W)

Na katika Riwaya hizi iwapo tutaangalia vyema tutagundua kuwa miongoni mwa maneno muhimu ya Mtukufu Mtume (s.a.w) kunako nafasi na daraja ya Imam Ali (a.s) ni, kauli ya Hadithi ya cheo (Manzilah) ambayo imezungumziwa zaidi kwa ndimi mbalimbali na marekebisho tofauti ya wapokezi, maulama wa Kiislamu na wanafiqh pia. Hadi ya cheo ni katika hadithi mashuhuri za Mtume inayokubalika na maulama wa Kishia na Kisuni.

Katika nukuu mashuhuri ya hadithi hii ni pale Mtume (s.a.w) alipomwambia Imam Ali (a.s):

«أنتَ مِنّى بِمَنزلةِ هارونَ مِنْ مُوسى، اِلّاأنـّه لانَبىَّ بَعدى».

"Wewe kwangu mimi ni mwenye cheo kama cha Harun kwa Mussa, ila tu hakuna nabii baada yangu”.[7]

Hadithi hii kadri ilivyo mashuhuri katika upokezi wake, matamshi yake, kwa uelewa wake katika nafasi zake na muda wake tofauti, mfano miongoni mwa muda wake ni siku ya kufunga undugu wa kwanza (kabla ya kuhamia Madina) na siku ya pili ya undugu (Miezi mitano baada ya kuhamia Madina), katika nyumba ya Ummu Salama, mashuhuri zaidi ni wakati wa vita vya Tabuk Mtume aliposema kauli hii,[8] lakini Muawiah anakanusha Hadithi hii, na pindi Sa’ad bin Abi waqqas alipoulizwa: Kwanini usimtusi Ali? Sa’ad akajibu: Ni kwa sababu ya fadhila tatu ambazo Mtume alizotaja kuhusu yeye. Wakati huo akamsomea hadithi ya Cheo na muawiah akamzuia kuendelea, ndipo akamuamuru Sa’ad kumlaani Imam Ali (a.s).[9]

Kwa hiyo baina ya Masahaba pia wako watu kama Sa’ad bin Abi waqqaas ambao pamoja na kumpinga kwao Imam Ali (a.s) na kutompa bai’a, basi alikuwa ni katika wale waliopokea hadithi hii, na vilevile wanatambua kuwa ni katika fadhila zake. Sa’ad ni katika wapokezi muhimu wa riwaya hii na watoto wa Sa’ad na wengine kama vile Said bin Musayyib na Bi Aisha wamepokea hadithi kutoka kwake.[10]

Katika hadithi hii pia tunaona kuwa nafasi ya Imam Ali (a.s) katika umma wa Kiislamu ni ileile nafasi ya Harun (a.s). hivyo kama vile Harun ameteuliwa na Mwenyezi Mungu kwa anuani ya Waziri na Khalifa wa Mussa (a.s), ndivyo ambavyo Imam Ali (a.s) alivyoteuliwa kwa anuani ya Waziri na Khalifa wa Mtume (s.a.w).

Mwenyezi Mungu katika Surat Taaha anasema kuashiria jawabu la ombi la Nabii Mussa (a.s) alipopewa amri ya kumlingania Firauni na watu wake, aliomba haya:

«وَاجْعَل لِي وَزِيراً مِنْ أَهْلِي ،هَارُونَ أَخِي، اشدد به ازری ، و اشرکه فی امری».

"Na nipe waziri katika watu wangu. Harun, ndugu yangu. Kwake yeye niongeze nguvu zangu”.[11]

Katika Aya hii imetubainikia kuwa, Nabii Harun (a.s) ni nduguye Nabii Mussa (a.s) na ambaye ni katika watu wa nyumbani kwake pia, aliyeteuliwa kuwa waziri, mshirika, msaidizi wa kazi za Nabii Mussa katika suala la kufikisha ujumbe wa Mwenyezi Mungu mtukufu.

5.               KIGEZO CHA MUUMINI NA MNAFIKI

Moja katika fadhila za Imam Ali (a.s) ni sifa na kigezo cha kuwa na Imamu, hadithi hii imejaa katika vitabu vya kishia na kisuni kutoka katika kauli za Mjumbe wa Mwenyezi Mungu (s.a.w), ikizungumzia fahari za Imam Ali (a.s) na iliyonukuliwa kwa mifumo tofautitofauti:

Amesema Mjumbe wa Mwenyezi Mungu (s.a.w):

«یا علیّ لا یُحِبّکَ الاّ مُؤمنٌ و لا یُبغِضُکَ الاّ مُنافِقٌ».

 "Ewe Ali! Hatokupenda isipokuwa ni Muumini na hatokuchukia isipokuwa ni Mnafiki”.[12]

Haarith Hamadaaniy anasema:

Siku moja nilimuona Ali (a.s) akipanda juu ya mimbari, na baada ya kumhimidi Mwenyezi Mungu na kusifu akasema:

«قضاءٌ قضاهُ الله تعالی عَلَی لِسانَ النّبی صلی الله علیه و آله، انّهُ قال: لا یُحبُّنی الاّ مؤمنٌّ و لا یُبغِضُنی الاّ مُنافقٌ وَ قَد خابَ مَنِ افتری».

Matakwa ya Mwenyezi Mungu mtukufu yaliyosemwa kwa ulimi wa nabii wake (s.a.w), ni kuwa amesema: "Hatonipenda Mimi ila ni mtu Muumini na hatonichukia Mimi ila ni mtu mnafiki, na amesema uongo atakayezua madai ya batili”.[13]

 

Sheikh: Juma. R. Kazingati.



[1] Bihaar al-anwaar, juz 40, uk 64, hadithi ya 98.

[2] Bihaar al-anwaar, juz 38, uk 27-40. Ibn Abil Hadid katika sharh yake, juz 9, mwisho wa hotuma ya 144. Al-ghadir, juz 3, uk 176.

[3] Bihaar al-anwaar, juz 38, uk 27-40. Ibn Abil Hadid katika sharh yake, juz 9, mwisho wa hotuma ya 144. Amesema: "Imenithibikia ya kuwa Mtume (s.a.w) amesema: Kwa hakika yeye iko pamoja na Haki iko pamoja na Yeye, inazunguka alipo Ali”. Al-ghadir, juz 3, uk 176.

[4] Aal imran/61.

[5] At-tawba/1.

[6] Shawaahid at-tanzil liqawaa’id at-tafsiil, juz 1, uk 159. Majma’ al-bayaan, juz 2, uk 696.

[7] Tafsir al-A’yyaash, juz 1, uk  332 na 153. Al-Aamal, cha sheikh Saduq, uk 63, hadithi ya 332. Bihar al-anwaar, juz 38, uk 332, hadithi ya 7. Ghaayat al-maraam, juz 2, uk 84, hadithi ya 21. Sahih al-bukhari, ,lango wa 9, uk 676-677, hadithi ya 3706.

[8] Ibn Hambal, juz 1, uk 277, juz 3, uk 513, 591. Sahih al-bukhari, juz 5, uk 129. Nasaai, uk 50-61. Ibn Kathir, juz 5, uk 87. Ibn Athir, juz 4, uk 104-105. Yanabi’I al-mawaddah, juz 1, uk 161.

[9]

[10] Khatib al-baghdadiy, juz 4, uk 642. Juz 5, uk 332. Juz 10, uk 499.

[11] Taaha/29-31.

[12] Al-irshaad, cha Sheikh Mufid, uk 18. Bihar al-anwar, juz 39, uk 310-246. Sahih al-muslim, juz 1, uk 48. Sawai’q ala-muhriqah, cha Ibn Hajar uk 120.

[13] Al-irshaad, cha Sheikh Mufid, uk 18. Bihar al-anwar, juz 39, uk 310-246. Sahih al-muslim, juz 1, uk 48. Sawai’q ala-muhriqah, cha Ibn Hajar uk 120. Sharh ibn Abil hadid, juz 18, uk 173, mwisho wa hekima ya 42.

LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: