bayyinaat

Published time: 16 ,December ,2017      20:08:20
Matatizo mengi sana katika mahusiano ya wana ndoa huanzia hapa, kwamba mume anaishi na mke wake kwa namna ambayo mwanamke hawezi kuhimili. Ukali, tabia mbaya n a mfano wa hayo........
News ID: 154

Ni jambo lililo wazi kabisa kwamba watu wawili wanapoamua kuingia katika mahusiano ya ndoa, basi kila mmoja alikuwa ameweka vigezo vya mwenza amtakaye ili aweze kuwa naye katika maisha hayo ya pamoja. Jambo la muhimu hapa na ambalo watu wengi sana huwa wanaghafilika nalo ni kuhusiana na kwamba je, unapoweka vigezo kwa ajili ya kupata mke au mume wa maisha yako, na ikatokea umempata, ndio huwa mwisho wa kila mmoja wenu kupambika na vigezo vile au la?.

        Bila shaka jawabu la kila mmoja wetu litakuwa ni hapana, kwa maana ya kwamba unapokuwa umechaguliwa na mwenza wako kwa ajili ya maisha ya pamoja basi huna budi kuendelea kujipamba na vile vigezo ambavyo kwavyo alikuchagua, kwa maana ikitokea akaona umebadilika n a huna tena yale mambo ambayo alikupendea basi itakuwa ndio mwanzo wa matatizo ndani y a ndoa yako.

Naomba nieleweke jambo moja hapa nisemapo kwamba inatakiwa uendelee kuwa na vigezo ambavyo kwavyo ulichaguliwa na mwenza wako, sina maana vigezo ambavyo sio msingi sahihi wa kuchagua, bali nakusudia vile vigezo sahihi ambavyo dini yetu ya Uislamu imetuambia tuviangalie kwa wenza wetu, kama vile dini, tabia njema na mfano wa hayo.

Sasa basi katika kuhakikisha kwamba mwanandoa anabakia katika vile vigezo vyake ambavyo vilifanya aweze kuchaguliwa, Uislamu haukubakia nyuma katika kuendelea kumpa nasaha huyu mwanandoa ili tu asije kughafilika.

Na leo tutachambua riwaya moja kutoka kwa Imamu Sadiq (as) ambayo anatuhusia kwamba tusije kudhania kwamba mume au mke baada tu ya kuwa pamoja na mweza wake basi anakuwa amekamilisha kila kitu, n a hana jambo lingine analotakiwa kulifanya katika ndoa yake hiyo, kwa maana hana hitajio lingine zaidi tu ya kuchukua mwenza. Hivyo basi msingi mzima wa mada hii ni kuhusiana na mambo ambayo kila mmoja kati ya mume na mke wanahitajia katika mahusiano yao haya yaliyobarikiwa.

Imamu Sadiq (as) anaanza kwa kusema:

لا غنى بالزوج عن ثلاثة أشياء فيما بينه وبين زوجته وهي:
الموافقة ليجتلب بها موافقتها ومحبتها وهواها . وحسن خلقه معها
واستعماله استمالة قبلها بالهيئة الحسنة في عينها وتوسعته عليها

"......Mume hatakiwi kujitosheleza  mambo matatu kwa mke wake, kuafikiana naye, ili tu aweze kuvuta mapenzi yake na pia awze kumfanya naye aafikiane naye, kuishi naye kwa tabia njema, na kuutawala moyo wake kwa njia ambayo itampendeza katika macho yake kama vile  kumuhudumia kadri ya uwezo......[1]

                           Ufafanuzi:

·       Hapa tunakuta Imamu (as) ameanza nasaha na wanaume kwanza, ikiwa na maana ya kwamba wasiwe ni vifua mbele tu katika mambo ambayo yanaelekea sana upande wao, bali hata kama si upande wao basi ni kwa kuwa wao ndio nguzo ya familia basi inatakiwa wayafanye kwa lengo la kuimarisha misingi ya mahusiano yao. Hivyo basi anatakiwa asiachane na mambo yafuatayo:

1.   Kuafikiana na Mke wake

Kwa maana ya kwamba ni lazima kuwe na maafikiano na kuendana baina ya wana mahusiano, na kuendana huku si tu katika mambo ya kidhahiri, bali pia iwe katika mambo ya kifikra, kiasi kwamba mume ajihisi yeye na mke wake ni kama mwili mmoja. Na faida ambayo imamu ameitaj akatika jambo hili ni kwamba bila shaka mke atakapoona kwamba mume wake ni mwenye kujipamba na hali kama hiyo, anamjali, anamchukulia kama mwili wake, anahuzunika na kufurahi naye, basi mke huyu naye atajibu mapigo kwa namna nzuri zaidi ambayo ni kumpenda na kuendana na mume wake kama ambavyo mume kaujenga msingi huu.

2.   Kuishi naye kwa mwenendo ulio mwema

Matatizo mengi sana katika mahusiano ya wana ndoa huanzia hapa, kwamba mume anaishi na mke wake kwa namna ambayo mwanamke hawezi kuhimili. Ukali, tabia mbaya n a mfano wa hayo. Inafika kipindi tukubali kwamba mke kama mke ameumbwa kwa kupenda kudekezwa, kuishi kwa upole na hali kadhalika, sasa mume anapokuwa hajachunga mambo haya, na akamfanya mke wake kama kijakazi wake na akaamua kuishi naye kwa hali ambayo mke ataihesabu ni kama ukali, hapo kutakuwa na tatizo bila shaka.

 

 

3.   Kuutawala moyo wa mke

Jambo hili kwa kweli linahitajia uelewa kwanza wa njia ambazo mke wako unaweza kuutawala moyo wake kwazo. Lakini Imamu hapa anaashiria jambo ambalo tukiliangalia basi bila shaka utakuta ni lenye kushirikiana kwa wanawake wote, hivyo basi kama wanaume watatumia jambo hili basi itakuwa ni silaha kubwa mno katika kuutawala moyo wa mke wake. Jambo lenyewe ni kumuhudumia mke wako, ndio, hakuna mwanamke ambaye hapendi kuhudumiwa na mumewe, kama ambavyo pia hakuna mwanaume ambaye anapenda kumuona mke wake akiwa rafu bila ya mpangilio mzuri wa kupendeza, hivyo basi mume inatakiwa ajitume kwa kadri ya uwezo wake ili tu aweze kufanikisha haya yote mawili, kwanza amuone mke wake katika hali nzuri ya kupendeza macho, n a kisha aweze kuuteka moyo wa mke wake kwa jambo hilo.

Na katika swala hili kuna maulama ambao wametoa fatwa kwamba ni Suna kwa mume kujipinda kwa ajili ya familia yake, pia hata Mtume (saww) ana maneno yake yasemayo "....Mwenye kufanya juhudi kwa ajili ya familia yake, ni sawa na mpiganaji jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu (swt)”.

Hivyo basi mume hana budi kushikamana na haya mambo ili tu aweze kudumisha na kuweka misingi mizuri ya maisha ya ndoa yake.

        Ungana nami katika wakati ujao ili tuweze kuona nasaha au mambo ambayo mke pia anatakiwa kushikamana nayo katika mahusiano yake na mumewe.

Sh Abdul Razaq Bilal.



[1] Tuhaful Uquul cha Ibn Shuubah Al Harraniy -ra- uk 323

maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: