bayyinaat

Published time: 06 ,March ,2017      14:06:46
Katika maswala ambayo yamekuwa yakizunguka katika vichwa vya Waislamu ni swala la kujadili na kutafuta ni nani ambaye anafaa kuwa Imamu na kiongozi wa Waislamu baada ya Mtume. Na ni kwanini Waislamu wamekuwa ni wenye haja na shauku sana katika kujadili jambo hili?. Kwani kuna sababu gani iliyopelekea mpaka.........
News ID: 39

Je uchambuzi juu ya swala la Uimamu ulianza lini?

Katika maswala ambayo yamekuwa yakizunguka katika vichwa vya Waislamu ni swala la kujadili na kutafuta ni nani ambaye anafaa kuwa Imamu na kiongozi wa Waislamu baada ya Mtume. Na ni kwanini Waislamu wamekuwa ni wenye haja na shauku sana katika kujadili jambo hili?. Kwani kuna sababu gani iliyopelekea mpaka kuanza kupatikana majadiliano na hata tafiti mbalimbali za nani ambaye anafaa kuwa Imamu baada ya mtume?.

Jawabu la swali hili tunaweza kulipata endapo tu tutarejea hali ya Waislamu baada ya kufariki dunia bwana Mtume Muhammad (saww), kwani ni jambo ambalo lipo wazi kwamba baada ya kufariki dunia tu Bwana Mtume (saww) umma uligawanyika makundi mawili makuu, na kila kundi moja likiwa na msimamo na itikadi yake juu ya ambaye anafaa kuwa kiongozi na Imamu baada ya Mtume (saww). Makundi hayo pamoja na misimamo yao ni kama ifuatavyo;

1.      Kundi ambalo linaamini kwamba Bwana Mtume hakuacha kiongozi baada yake, na kwamba swala la umma kuwa na kiongozi lipo mikononi mwa umma na Waislamu wenyewe, wao ndio wana haki ya kumchagua wamtakaye ili awe kiongozi na Imamu wao.

2.      Kundi ambalo linaamini kwamba kazi ya kuchagua kiongozi wa Waislamu baada ya Mtume ipo mikononi mwa Mwenyezi Mungu (swt), kwani huyu kiongozi ni lazima awe na sifa ambazo alikuwa nazo yule aliyekuwa kabla yake mfano sifa ya kutofanya madhambi na nyinginezo, na kwakuwa sisi wanadamu hatuna uwezo wa kuweza kutambua kwamba huyu ana sifa hizo au la, inakuwa kwamba ni lazima Imamu na kiongozi huyu aainishwe na Mwenyezi Mungu kupitia Mtume wake.

Hivyo basi na sisi katika mada hii tutajaribu kufuatilia jambo hili kwa ukaribu mno na kuweza kufikia katika natija sahihi huku tukitumia Quran, Sunna pamoja na historia sahihi ya Uislamu, lakini kabla ya kuanza hilo ni lazima tutambue baadhi ya mambo muhimu ambayo ni mwongozo wa kutambua jambo hili. Mambo yenyewe ni yafuatayo:

a.     Je, ni kweli kuzungumzia jambo hili husababisha tofauti baina ya Waislamu?.

imekuwa ni jambo lenye kuzoeleka sasa katika jamii zetu kwamba, kili isikikapo jambo la kujadili juu ya Imamu na kiongozi wa Waislamu baada ya Mtume basi watu wote husimama na kusema kwamba jambo hili halifai kujadiliwa wakati huu, kwani huu ni muda wa Waislamu kushikamana na kuwa wamoja, na kwamba swala la kujadili Uimamu baada ya Mtume ni katika mambo ambayo husababisha mfarakano na mgawanyiko wa Waislamu. Lakini sidhani kama mtazamo huu ni sahihi kabisa, na hii ni kutokana na sababu zifuatazo:

Kwanza: jambo ambalo husababisha mfarakano na mgawanyiko na hata chuki baina ya Waislamu ni kujadili mambo haya hali ya kuwa kila mmoja hana moyo safi wa kutaka kuelewa au kujua ukweli, bali unakuta kwamba mtu anajadili jambo hili huku moyo ukiwa haupo tayari katika kusikia au kukubali ukweli, sasa inapotokea akaambiwa ukweli upo hivi na hali ya kuwa moyo wake hautaki kusikia na kuamini kwamba hayupo sahihi hapo ndipo ambapo mfarakano unapatikana. Na wala haiwezekani mfarakano ukapatikana endapo kila mmoja ataingia katika mjadala wa jambo hili huku akiwa na moyo safi wa kuwa tayari kukubali ukweli hata kama utakuwa dhidi yake.

Pili: inawezekana sababu ya mfarakano baina ya Waislamu ikawa ni kutofahamiana wao kwa wao, kwa maana ya kwamba utakuta kundi hili lina amini imani fulani na dalili zake zikawa ni fulani, lakini maadui wa Uislamu wakasimama kidete kuhakikisha kwamba zile dalili zinabadilishwa maana yake na kupelekwa upande wa pili ambao hauamini ambayo yanaaminiwa na upande wa kwanza. Kwa mfumo huu bila shaka lazima kutakuwa na mizozo ya kwanini na kwanini huku ikidhanika kwamba sababu ya mizozo ile ni kujadili tu maswala mfano wa swala hili la Uimamu.

Mfano mzuri ni ule ambao tunakutana nao kila siku katika maisha yetu, ambapo tunakuta kwamba kuna kundi la Waislamu linalojitahidi kuaminisha umma kwamba, baina ya Waislamu kuna ambao wana Quran yao tofauti na Quran iliyozoeleka kwa Waislamu wote. Sasa mambo kama haya hua ndio sababu ya mizozo na mifarakano kwa Waislamu na sio kujadili mambo yanayohusu Uislamu kwa moyo safi na nia njema.

b.    Nini maana ya Uimamu?

Imamu kama ambayo inaelezwa maana yake ni yule ambaye anafuatwa katika Uislamu na yeye anawaongoza wanaomfuata. Isipokuwa tu itakuja tofauti kwa upande wa dhehebu la Shia (ithna asharia)  kwamba wao wanaamini ya kuwa huyu Imamu ni lazima awe ni maasumu (ambaye hafanyi dhambi) na kwamba Imamu huyu maasumu haina maana kwamba atakuwa ni kiongozi katika mambo ya dini tu, bali anakuwa ni kiongozi katika kila jambo ambalo linawahusu Waislamu. Na hii ni maana ambayo hatuipati katika dhehebu nyingine za Kiislamu, kwani wao huamini kwamba Imamu au kiongozi wa Kiislamu anakuwa ni kiongozi wa jamii ya Kiislamu na maswala ya kidini tu, ama mambo mengineyo yanakuwa nje ya utawala na mikono yake.

ndugu msomaji mpaka kufikia hapa tunakuwa tumeweza kutambua ni ipi maana ya Imamu, kama ambavyo pia tunakuwa tumeweza kutambua kwamba swala la kujadili Uimamu si katika maswala ambayo husababisha tofauti baina ya Waislamu, lakini ni kwa sharti tu kwamba swala hili lijadiliwe hali ya kuwa tupo na nia safi na moyo wa kukubali ukweli hata kama utakuwa dhidi yetu.

Tukutane katika makala ijayo kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu.

 

LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: