bayyinaat

Published time: 07 ,March ,2017      20:58:04
Lakini ndugu msomaji, swala la muhimu kujua hapa ni kwamba, Uislamu ambao unamaanishwa na pia ulikuwa katika kila dini ni upi? Maana isije tukaelewa vibaya na mwisho wake tukaangukia katika janga kubwa la kupinga dini nyinginezo na kusema kwamba hazijulikani kwa Mwenyezi Mungu.......
News ID: 43

Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na mwenye kurehemu

Mahusiano baina ya Uislamu na dini zilizopita

Miongoni mwa neema kubwa ambazo Mwenyezi Mungu amewajaalia waja wake, ni kwamba amewaumba katika hali ya kwamba wao ndani ya nafsi zao wana hali ya kumjua na kumkubali Mungu, na hali hii ipo kwa kila mwanadamu hata kama atakuwa ni mwenye kupinga kwa maneno au matendo yake, lakini ni kwamba kimaumbile ni mwenye kukubali uwepo wa nguvu iliyo juu ya kila kitu. Lakini kutokana na kwamba hali hii ni hali ambayo bado haijafafanuliwa zaidi kwa mwanadamu huyu ndio tunakuta kwamba mwenyezi mungu anatuma Mitume ili kuja kuisherehesha hali hii pamoja na kuthibitisha kwamba ni kweli ipo isipokuwa ili uitambue ni lazima upite katika misingi fulani. Na miongoni mwa misingi hiyo ni kama:

1.     Kumpwekesha Mungu na kutomshirikisha na yeyote

2.     Kumuabudu yeye peke yake pasi na mwingine

3.     Kulinda na kuhifadhi mambo ya watu pamoja na kutosababisha uharibifu

4.     Kulingania watu kuelekea katika tabia zilizo bora. Na mfano wa mambo mengine mengi ambayo huja kuelekezwa na Mitume.

Kisha Mwenyezi Mungu kwa matakwa yake akaamua kwamba dini ya Islamu iwe ndio dini ya mwisho na ambayo inakuja kukamilisha dini zote zilizopita, na kwamba dini zilizopita au mitume pamoja na ujumbe zao ni kwamba zilikuwa na muda maalumu tu. Lakini hii haina maana kwamba dini ya Islamu ni dini ambayo imekuja kupinga na kubatilisha dini zilizopita, au kuja kusema kwamba dini hizo hazikuwa na maana wala mashiko, na ndio maana katika makala hii tunataka kubainisha kwamba Uislamu kama Uislamu una mambo ambayo yanashikamana na yanaendana na dini zilizopita, kwani lengo la Uislamu ni kuja kukamilisha dini zote zilizokuwa kabla yake. Na mambo hayo ni kama ifuatavyo:

1.    Msingi na asili ya dini zote ni moja

hii ikiwa na maana kwamba, pamoja na kuwa dini hutofautiana zama na nyakati au hata Mtume ambaye huja nayo, ila tunakuta kwamba dini hizi zote zinakutana katika asili na msingi. Na msingi huo ni kwamba zote zinatoka kwa Mwenyezi Mungu mmoja, (lakini hapa ni lazima ifahamike kwamba dini tunazozikusudia ni dini ambazo zinatoka kwa mwenyezi mungu na sio dini za kuundwa na wanadamu wenyewe) na katika kubainisha hilo tunakuta Mwenyezi Mungu anasema:

شَرَعَ لَكُمْ مِنَ الدِّينِ مَا وَصَّىٰ بِهِ نُوحًا وَالَّذِي أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ وَمَا وَصَّيْنَا بِهِ إِبْرَاهِيمَ وَمُوسَىٰ وَعِيسَىٰ ۖ أَنْ أَقِيمُوا الدِّينَ وَلَا تَتَفَرَّقُوا فِيهِ ۚ ....

" Na amekuwekeeni sheria ambayo aliiweka kwa Nuh, na hayo ndio ambayo tumekupatia wewe na Ibrahimu na Mussa na Issa (Yesu)  ya kwamba muwe ni wenye kusimamisha dini na wala msiwe ni wenye kutofautiana......” surat Shuura aya ya 13.

Kwa hiyo kwa msingi huu ni kwamba imani ya kweli haiwi tu kwa kusadikisha yale ambayo amekuja nayo mtume wa zama zako, bali pia ni kusadiki ambayo walikuja nayo mitume wa kabla pia.

2.    Malengo ya dini zote ni mamoja

Hapa ikiwa na maana kwamba dini zote pamoja na kutofautiana kwake nyakati na muda, ila zinakuja kukutana katika malengo yake. Kwani kama ambavyo ipo wazi ni kwamba dini zote zinakuja kwa lengo la kumwongoza mwanadamu na kuhakikisha kwamba anafikia katika ukamilifu ambao kwao aliweza kuumbwa.

 

3.    Dini zote zina nembo ya Uislamu

Naam na wala sio uongo, kwani ni jambo ambalo tunalikuta kwa Mitume iliyopita pia tofauti na mtume Muhammad (saww), na hii ndio maana ya kauli ya Mwenyezi Mungu aliposema  :

إِنَّ الدِّينَ عِنْدَ اللَّهِ الْإِسْلَامُ 

"hakika dini mbele ya Mwenyezi Mungu ni Uislamu”

Al imran aya ya 19.

Na ili kuthibitisha ya kwamba hata katika dini za mitume iliyopita kulikuwa na nembo ya Uislamu, yatutosha kurejea kauli za baadhi ya mitume walipokuwa wakielezea malengo na falsafa ya dini walizokuja nazo. Angalia mtukufu nabii Nuhu katika maneno yake baada ya kubainisha malengo yake anasema:

وَأُمِرْتُ أَنْ أَكُونَ مِنَ الْمُسْلِمِينَ

"na nimeamrishwa niwe ni mwenye kujisalimisha (Mwislamu)

Surat Yunus aya 72

 

 

Pia tunamkuta Nabii Yusuf katika dua alizokuwa akiomba ni pale aliposema:

تَوَفَّنِي مُسْلِمًا وَأَلْحِقْنِي بِالصَّالِحِينَ 

"ewe mola wangu nifishe hali ya kuwa nikiwa Mwislamu na uniweke pamoja na walio wema” surat Yusuf aya ya 101.

Na kauli nyingi mno ambazo zimepokelewa kwa Mitume wengine kama vile Suleiman, Ibrahim, Ismail, Yakob na wengineo, kauli ambazo zote zina maana ya kuashiria kwamba katika ujumbe wao kulikuwa na nembo ya Uislamu.

Lakini ndugu msomaji, swala la muhimu kujua hapa ni kwamba, Uislamu ambao unamaanishwa na pia ulikuwa katika kila dini ni upi? Maana isije tukaelewa vibaya na mwisho wake tukaangukia katika janga kubwa la kupinga dini nyinginezo na kusema kwamba hazijulikani kwa Mwenyezi Mungu.

Ili kuweza kujua na kufahamu maana ya Uislamu ambao ulikuwa katika kile dini basi usiache kuungana nami katika makala ijayo kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu (swt)

Sh Abdul Razaq Bilali.

 

LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: