bayyinaat

Published time: 07 ,March ,2017      21:25:13
Miongoni mwa mafunzo ya dini tukufu ya Kiislam ni 'usafi wa kimwili na kiroho'. Naamini kwamba kila mtu atakuwa wa kwanza kukubaliana na mimi katika kauli hii kwamba 'dini tukufu ya Kiislam ni dini safi'. suala hilo liko wazi mno kwa wanadamu wote waliotangulia waliopo na watakao fuatia. Na ndio maana utaikuta dini hii inasisitiza zaidi usafi.....
News ID: 44

MWENYEZI MUNGU (S.W) KAMFADHILISHA MWANADAMU

                                     ' KWA FADHILA YA USAFI

Ndugu msomaji, kwa hakika kama ambavyo akili huweza kumtofautisha mwanadamu na viumbe wengine, hivyohivyo usafi. Na hii ni miongoni mwa fadhila kubwa alizobahatika kufadhilishwa kwazo mwanadamu kuliko viumbe wengine kama alivyosema Mwenyezi Mungu (s.w):

﴿وَفَضَلناهُمْ على كثيرٍ مِما خلقنا تفضيلاً

"na tumewafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa tulio waumba"

Miongoni mwa mafunzo ya dini tukufu ya Kiislam ni 'usafi wa kimwili na kiroho'. Naamini kwamba kila mtu atakuwa wa kwanza kukubaliana na mimi katika kauli hii kwamba 'dini tukufu ya Kiislam ni dini safi'. suala hilo liko wazi mno kwa wanadamu wote waliotangulia waliopo na watakao fuatia. Na ndio maana utaikuta dini hii inasisitiza zaidi usafi.

Allah (s.w) baada ya kumuumba mwanadamu kwa maumbile mazuri na sura nzuri kama zisemavyo Aya tukufu akaendelea kumkirimu mwanadamu huyu kwa kumuumbia vitu ambavyo kwavyo mwanadamu anaweza kutengeneza mavazi au nguo ili ahifadhi mwili wake, anasema Allah (s.w):

﴿يا بَنِي آدَمَ قَدْ أَنزَلْنَا عَلَيْكُمْ لِبَاساً يُوَارِي سَوْءَاتِكُمْ وَرِيشاً

"Enyi wanaadamu! Tumekuteremshieni nguo za kuficha tupu zenu, na nguo za pambo…."

( Qur`an-7/26).

Mwenyezi Mungu hakufanya hivyo isipokuwa alitaka mwanadamu huyu aonekane katika mandhari iliyokuwa nzuri ili aende sawia na maumbile yake, na ili kumtofautisha na viumbe wengine ambao hawakubahatika kuteremshiwa nguo (kama isemavyo Aya hii) au kuumbiwa vitu ambavyo wanaweza kutengeneza nguo kutoka katika  vitu hivyo ili wahifadhi miili yao.

Na iko wazi kwamba uzuri wa dhahiri ya mwanadamu hautakamilika pasina kulitilia umuhimu usafi, kama ambavyo uzuri wa batini (au uzuri wa nafsi) haupatikani pasina kulitilia umuhimu uchamungu ambao maana yake ni "kutii amri zote za Mwenyezi Mungu (s.w) pamoja na kuacha yote aliyokukataza Mola wako".

 Ili uwe msafi zaidi kiroho ni lazima uwe mchamungu kwa maana hiyo tuliyoitaja hivi punde. Na hivyohivyo ndivyo usafi wa dhahiri au mwonekano wa nje wa mwanadamu hupendeza kwa kutilia umuhimu usafi wa mwili, kwa maana kwamba unatakiwa uwe na tabia ya kupenda kuvaa nguo nzuri na safi, uwe na tabia ya kupenda kulala katika sehemu iliyokuwa safi, na uwe na tabia ya kupenda kuishi katika sehemu iliyokuwa safi yenye mazingira safi.

Hivyo usafi kwa mwanadamu tutauzungumzia katika sekta hizi zifuatazo:

Usafi kwa mtu binafsi (mwili wake na mavazi yake).*

*Usafi katika jamii yake anayoishi

*Usafi katika taifa lake.

USAFI UNAOMHUSU MTU BINAFSI

Tumesema kwamba miongoni mwa neema za Mwenyezi Mungu (s.w) kwa Mwanadamu ni kumtakasa mwanadamu huyu na kumfanya awe msafi kuanzia usafi wa kiroho (au usafi wa bitini na wa ndani ya nafsi), hadi usafi wa kimwili (nikimaanisha usafi wa dhahiri wa mwanadamu).

Katika Suuratul Maidah, Aya ya 6, Mola wetu Mtukufu anasema:

﴿مَا يُرِيدُ اللـه لِيَجْعَلَ عَلَيْكُم مِنْ حَرَجٍ وَلكِن يُرِيدُ لِيُطَهِّرَكُمْ وَلِيُتِمَّ نِعْمَتَهُ عَلَيْكُمْ لَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ

"Mwenyezi Mungu hataki kukutieni katika taabu; bali anataka kukutakaseni na kutimiza neema yake juu yenu ili mpate kushukuru"

Dini tukufu ya Uislamu inasisitiza usafi wa aina zote mbili, kwamba Mwislamu anatakiwa kuwa msafi kiroho, kwa kuilea nafsi yake iwe ni yenye kumtii Mwenyezi Mungu (s.w) katika mambo yote pasi na kwanini, pia iwe ni nafsi yenye kuheshimu haki za wengine na kuishi na watu vizuri, nafsi isiyokuwa na chuki wala kinyongo, iwe ni nafsi yenye uwezo wa kusamehe inapokosewa na kuomba msamaha inapokosea, nafsi yenye huruma, upole na ustahamilivu, n.k., na hivyo ndivyo usafi wa kiroho unavyotimia.

Ama kuhusiana na usafi wa dhahiri ambao ndio muhimili mkubwa wa mada hii  Uislamu unahimiza siku zote Mwislamu azingatie usafi wa mwili wake, na hata nguo zake anazozivaa pamoja na chakula chake anachokula, tunatakiwa kuhakikisha  vyote hivyo vinakuwa katika hali ya usafi.

Mwanadamu (Mwislamu) kama unavyotakiwa kuwa msafi wa kimwili na mavazi yako hivyohivyo ndivyo unatakiwa kula chakula bora na safi kilichohalalishwa ,na hili ni miongoni mwa mambo ambayo Allah (s.w) amemtaka Mtume Muhammad (s.a.w.w) ayafanye.

ukirudi katika historia ya maisha ya Mtume (s.a.w.w) utakuta ni Mtume ambaye hakutosheka na kuwaamrisha wanadamu mema na kuwakataza maovu tu, bali pia alifanya kazi kubwa ya kuwabainishia na  kuwahalalishia vilivyokuwa halali na safi, na kuwaharamishia kinyume na hivyo, katika Suuratul Aa'raf,Aya ya 157 Mwenyezi Mungu (s.w) anasema namna hii:

 ﴿وَيُحِلُّ لَهُمُ الطَّيِّبَاتِ وَيُحَرِّمُ عَلَيْهِمُ الْخَبَآئِثَ

"…..  na anawahalalishia vitu vizuri, na kuwaharamishia vitu vichafu"

Kunako usafi wa mwili ni pamoja na kuzingatia suala la kuoga, kuweka nywele zako safi, kukata au kupunguza kucha ,kuzingatia suala la kupiga mswaki ,kweka kiatu chako safi, pamoja na mavazi yako (au nguo zako) kuonekana katika mpangilio uliokuwa mzuri. n.k.

Ikiwa wewe ni Mwislamu anayependa na kutarajia kuingia peponi ,basi zingatia usafi wa ndani ya nafsi yako, usiwe kiburi katika nafsi yako maana utakuwa unaichafua kwa kufanya hivyo, pia unatakiwa uzingatie usafi wa kimwili ,kwa kuvaa mavazi safi na kiatu chako unapiga dawa king'ae ,kwa kufanya hivyo utakuwa unamfurahisha Mwenyezi Mungu( s.w) na bila shaka ukimfurahisha Mola wako utakuwa umefanikiwa kuingia kwenye orodha ya wale watakao ingia Peponi, kwani  pepo ya Allah (s.w) ni safi na watakaoingia ndani yake ni wale waliozingatia usafi .Na hivi ndivyo alivyosema Mtume (s.a.w.w), Ibn Mas-uud amesema kwamba Mtume (s.a.w.w) amesema:

( لا يدخل الجنة من كان في قلبه مثقال ذرة من كبر، فقال رجل: إن الرجل يحب أن يكون ثوبه حسنا ونعله حسنا، قال –يعني النبي صلى الله عليه واله وسلم-: إن الله تعالى جميل يحب الجمال، الكبر بطر الحق، وغمط الناس.)

"Hataingia peponi yeyote atakaye kuwa na chembe ndogo ya kiburi katika moyo wake, Mtu mmoja (akashangaa sana alivyosikia kauli hii ya mtume -s.a.w.w.-mana yeye alikielewa kwamba kuvaa nguo nzuri na safi, pamoja na kuvaa kiatu safi ni aina moja wapo ya kiburi) akamuuliza Mtume s.a.w.w- kwa kusema: Kuna Mtu (fulani) ana tabia ya kupenda nguo zake ziwe safi,  pia anapenda kiatu chake kiwe safi!,

(Vipi mtu huyu, naye hataingia peponi?), Mtume (s.a.w.w) akamjibu kwa kusema:

Hakika Mwenyezi Mungu ni msafi, na anapenda usafi, kiburi ni majivuno na maringo yaliyo dhidi ya haki kwani humfanya mtu awe na dharau na kutokuwa tayari kuitambua haki ya mtu mwingine"

Mwenyezi Mungu anapokuwa amekuneemesha kwa neema fulani, basi hupendezwa sana kuziona athari nzuri za neema hiyo aliyokupa, kwa mfano neema ya akili, atafurahi sana Mola kuona ikiwa utaitumia akili yako vizuri ,na hivyohivyo ikiwa utazingatia usafi hakika Mola wako atafurahi mno kuona ni jinsi gani unavyoithamini neema yake ya kukuumba vizuri na kukupa sura nzuri ikiwa utajali usafi wa maumbile yako (mwili wako).

Itendelea.......
Sh Taqee Zakaria
LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: