bayyinaat

Published time: 07 ,March ,2017      21:32:11
Hivyo basi tunatakiwa kuvaa vizuri, nguo safi, zinazopendeza na kutufanya tuonekane vizuri, ikiwezekana unatia na manukato hasa unapokuwa mbele ya Mola wako ukifanya ibada, itapendeza sana ikiwa utaingia katika swala ukiwa msafi mwenye mavazi safi, na hivi ndivyo Waislam tunavyotakiwa tuwe, kwani amesema.....
News ID: 45

Hivyo basi tunatakiwa kuvaa vizuri, nguo safi, zinazopendeza na kutufanya tuonekane vizuri, ikiwezekana unatia na manukato hasa  unapokuwa mbele ya Mola wako ukifanya ibada, itapendeza sana ikiwa utaingia katika swala ukiwa msafi mwenye mavazi safi, na hivi ndivyo Waislam tunavyotakiwa tuwe, kwani amesema:

 

 

 ﴿ يَا بَنِي آدَمَ خُذُواْ زِينَتَكُمْ عِندَ كُلِّ مَسْجِدٍ وكُلُواْ وَاشْرَبُواْ وَلاَ تُسْرِفُواْ إِنَّهُ لاَ يُحِبُّ الْمُسْرِفِينَ﴾

"Enyi wanaadamu (Waislamu)! Chukueni pambo lenu kwenye kila pahala wakati wa ibada, na kuleni (vizuri), na kunyweni (vizuri) na wala msifanye ubadhirifu, Kwa hakika Yeye hapendi wabadhirifu".

 

Hivyo itakuwa ni suala la msingi ikiwa tutaitumia neema ya maji tuliyopewa na Mola wetu kwa kufanya usafi wa mwili na mavazi, kama kuoga, kufua nguo zetu, n.k. na iwapo hatutafanya hivyo basi tujue kwamba badala ya kumfurahisha Mola wetu tutakuwa tunamuudhi.

Imepokewa riwaya kutoka kwa Jaabiri anasema kwamba ;

"أتانا رسول الله صلى الله عليه وسلم زائراً، فرأى رجلا شعثاً، قد تفرق شعره، فقال: ما كان يجد هذا ما يسكن به رأسه"

"siku moja tulimzuru Mtume (s.a.w.w), Mtume akamuona mtu (miongoni mwa waliomjia) ambaye nywele zake zilikuwa zimatawanyika tawanyika,akasema kwa kuuliza (s.a.w.w): Mtu huyu hakupata kitu cha kumuwezesha kuziweka nywele zake safi zikatengamaa"?!.

Pia amepokea Abi Ahwaswi kutoka kwa baba yake kuwa amesema:

( أتيت رسول الله صلى الله عليه واله وسلم وعلي ثوب درن، فقال لي: "ألك مال"، قلت نعم. قال: من أي المال؟ قلت من كل المال، قد أعطاني الله من الإبل والغنم والخيل والرقيق. قال: فإذا آتاك الله مالا فلير أثر نعمة الله عليك وكرامت.)

"Nilimjia Mtume (s.a.w.w) ilihali katika nguo yangu kukiwa na uchafu, Mtume akaniambia: Una mali?, nikasema: ndio, akasema (s.a.w.w):ni mali zipi ulizokuwa nazo?, nikasema: mali zote, kwa hakika Mwenyezi Mungu -s.w- amenipa (mifugo mingi sana) Ngamia, Kondoo na Mbuzi, Farasi pamoja na watumwa. Mtume (s.a.w.w) akasema: Mwenyezi Mungu anapokupa mali basi jitahidi sana aone athari za neema zake alizokupa pamoja na fadhila zake kwako."

Riwaya hii inatubainishia ni jinsi gani suala la usafi lilivyopewa umuhimu mkubwa katika Uislamu, ukiwa mchafu wa mavazi basi utakuwa si mwenye kushukuru neema za (Mwenyezi Mungu (s.w) ,kwani unaweza kujali mwili na kuuweka katika hali ya usafi lakini hufanyi hivyo ,kakupa maji na unaweza kuoga na kufua nguo zako na kuziweka safi lakini hufanyi hivyo, na hakuna shaka kuwa kufanya hivyo ni kukufuru neema za mola wako.

Na usafi sio wa mwili peke yake bali pia tunatakiwa tufanye usafi kwenye majumba yetu na sehemu tunazoishi, tuyapambe majumba yetu kwa usafi yawe mazuri, mazingira yetu yavutie, tukifanya hivyo basi tutakuwa ni miongoni mwa wale ambao Allah (s.w) amewazungumzia kwa kuwasifu akisema :

﴿ فِيهِ رِجَالٌ يُحِبُّونَ أَن يَتَطَهَّرُوا وَاللـه يُحِبُّ الْمُطَّهِّرِينَ

…..Humo wamo watu wanao penda kujitakasa (na kuwa wasafi), na Mwenyezi Mungu anawapenda wanaojitakasa".

(Tazama katika Suratut- Tawbah: Aya ya 108.)

Katika Aya  hii Mwenyezi Mungu anazungumzia kunako tohara na usafi kwa ujumla, hivyo ili tufanikiwe na kuwa miongoni mwa wale wanaopendwa na Mola wao ,tunatakiwa tupende usafi na tupende kuwa wasafi.

USAFI WA JAMII

Ikiwa Mtu au Mwislamu atazingatia usafi unaomhusu yeye binafsi kuanzia mwili wake na mavazi yake n.k, basi ataweza kuzingatia usafi wa jamii yake anapoishi. Na usafi wa jamii ni tofauti na usafi wa kimwili unaohitaji vitu kama kuoga ,kuvaa nguo safi na nzuri kuweka nywele safi kukata kucha n.k, bali katika sehemu hii ninaposema usafi katika jamii ningependa kumaanisha usafi wa mazingira katika jamii unayoishi.

Hakikisha mazingira ya jamii yako yawe safi, na uchukie utakapomuona mtu anachafua mazingira maana atakuwa anaichafua jamii yako.

Kuna watu utakuta wana tabia ya kuchafua mazingira ,kama vile kujisaidia hovyo sehemu zisizotakiwa ,pia kuna watu wengine hawajui nini maana ya kutunza mazingira, ni waharibifu wa mazingira, kwa hakika hali hii hutokana na kutojua au kutambua thamani ya utunzaji wa mazingira ,mtu wa namna hiyo itakuwa ni vigumu kwake kutunza hata usafi wa mwili wake.

Msafi ni yule ambaye usafi wake hauishii kujali mwili wake na kuvaa vizuri, bali msafi ni yule ambaye hupenda kuwa safi yeye binafsi pia mazingira ya jamii yake. utamkuta mtu ni mwenye kufanya usafi hata wa njia na sehemu wanazo pumzikia watu, maana anajali, hajisikii furaha kuona njia ikiwa na miba, ama mchafu yeye hana habari na hajali , bali utamkuta ni bingwa wa uchafuzi wa mazingira na njia za watu, kwa hakika ada mbaya sana ni mtu kutupa takataka kwenye njia za watu, mwenye kuchafua barabara ambapo husababisha njia hizo kuwa na harufu mbaya inayokera watu, yeyote atakayefanya hivyo basi ajue kwamba anailetea maudhi jamii yake, na nchi yake kwa ujumla.

                                                                                                                                    

Mtume (s.a.w.w) anatwambia kwamba:

                                                                                                                  

(التسبب في اتساخ الطريق وأذى المارة سيئة تنقص من درجة الإيمان الكامل)

" kusababisha uchafu katika nchi na kuwaudhi wapita njia ni jambo baya sana ambalo linapunguza daraja ya imani kamili,".

Mtume (s.a.w.w) anasema:

" أتقو اللاعنين ، قيل : وما اللاعنان؟ قال : الذي يتخلىّ في طريق الناس أو ظلهم "

"Jitenge na walio laaniwa Wawili, Mtume akaulizwa: ni watu gani hao wawili walio laani: Mtume (s.a.w.w) akasema: Anayejisaidia katika njia wapitazo watu au anayejisaidia katika sehemu za vivuli vya watu kwa ajili ya kupunga upepo na kupumzika

 itaendelea…:

Sh: Taqee  Zakaria.
LABEL:
maoni Viewers
Name:
Email:
* Opinion: