SEHEMU YA
KWANZA
Nini maana ya
tamaduni, na je neno (tamaduni) hutumika mahala gani?
Katika kuelezea maana halisi ya neno
"tamaduni” kumekuwa na kauli na rai mbalimbali ambazo zote zina lengo moja la
kuweza kubainisha na kuweka sawa maana halisi ya neno hili. Na hapa tutajaribu
kuleta baadhi ya kauli na rai hizo, kisha tuone ni kitu gani ambacho kinalengwa
na kauli na rai hizo kwa pamoja.
MAANA YA KWANZA
Baadhi ya wataalamu wa masuala yanayohusiana
na tamaduni, wamejaribu kuelezea maana ya neno "tamaduni” kuwa ni : namna na
jinsi ambavyo mwanadamu anakabiliana na maisha katika mazingira yake.
Kwa maana ya kwamba kunakuwa na
mambo matatu muhimu katika maana hii, kwanza na mwanadamu na kisha ni mazingira
na mwisho kabisa ni maisha anayoishi na namna ambavyo anakabiliana na kila
jambo linalojitokeza katika maisha hayo. Sasa njia na namna ambazo anazitumia kukabiliana
na changamoto au maisha yake kwa ujumla ndio huitwa tamaduni. Na kitu cha
muhimu katika maana hii ni namna ambayo hutumika katika kukabiliana na maisha
husika.
MAANA YA PILI
Wataalamu wengine wa maswala ya
kijamii na tamaduni husika kwa ujumla, wanajaribu kuelezea maana ya tamaduni
kwa kusema: ni mkusanyiko wa watu maalumu na ambao huishi katika mazingira
maalumu huku wakiwa ni wenye kuendelea katika sekta ya uandishi. Kwa maana ya
kwamba ili kuwe na tamaduni basi ni lazima kwanza kupatikane watu maalumu, na
watu hawa wawe ni wenye kuishi katika mfumo maalumu, na kisha ni lazima watu
hawa wawe ni wenye kuendelea katika sekta ya uandishi, kwa maana ya kwamba bila
ya kuwa na mwendelezo katika nyanja ya uandishi basi hakuwezi kuwa na tamaduni.
MAANA YA TATU
Wataalamu waliokuja na maana hii,
hawakuwa mbali sana na wale waliokuja na maana ya tatu kwamba, ni lazima kuwe
na watu maalumu ambao wanaishi katika mazingira maalumu, na wawe ni wenye
kuendelea katika sekta ya uandishi, ila tu wataalamu hawa wamekuja na kitu cha
ziada ambacho ni: ili iwe ni tamaduni, basi ni lazima watu hawa maalumu wawe ni
wenye elimu au ujuzi kuhusiana na watu waliopita pamja na historia zao.
Kwa maana ya kwamba sawa wanatakiwa
wawe ni wajuzi katika sekta ya uandishi, lakini ujuzi huu wanautumia wapi? Moja
ya sehemu husika au moja ya sehemu zinazotumia ujuzi huo ni kuweza kunakili na
kudhibiti taarifa muhimu za watu waliopita pamoja na jinsi walivyokuwa wakiishi
au kukabiliana na maisha katika sehemu yao.
Kwa maana hii basi, kitu cha muhimu
zaidi ni kwamba watu hawa ni lazima wawe na ujuzi na elimu ya kuhusiana na watu
waliokuwa kabla yao, wao na jinsi walivyokuwa wakiishi.
MAANA YA NNE
Hii ni maana ambayo imekuja kuletwa
na wataalamu wa maswala ya lugha na kisha kuweza kuitumia kama maana sahihi ya
neno "tamaduni”.
Ambapo wataalamu hawa wanatuambia
kuwa tamaduni ni neno lenye asili ya Kiarabu ambalo ni "مدن” "madana” likiwa na maana ya "aliishi
sehemu fulani”, kwa hiyo neno "tamaduni” linakuwa na maana ya "kuishi katika
sehemu fulani” bila ya kuwa na sharti wala kitu cha ziada ili kuweza kuleta
maana ya neno hili kama ambavyo wataalamu waliokuja na maana za juu
wameashiria. na kutokana na maana hii
ndipo wakaja na maana ya neno "tamaduni” kuwa ni kitendo cha mwanadamu kuwa ni
mwenye kuishi katika mazingira fulani.
Sasa hizi
zote ni maana ambazo wataalamu wa maswala ya tamaduni na lugha kwa ujumla
wanajaribu kutueleza ili tufahamu maana ya neno
"tamaduni”. Lakini kama tutakuwa tumezingatia maana zote hizo ambazo
tumezileta hapo juu, bila shaka tutakuwa tumegundua kuwa kuna baadhi ya mambo
ambayo tunaweza kuyakusanya pamoja, na hii ni kutokana kwamba mambo hayo yote
japokuwa yameletwa na wataalamu mbalimbali, lakini kwa pamoja yanalenga maana
moja. Kwa mfano tumeweza kushuhudia katika maana zote kwamba:
Moja:
tamaduni ni lazima wawe watu ndio wanahusika na sio viumbe wengine.
Mbili: watu
hawa ni lazima wawe wanaishi katika mazingira maalumu yanayofanana.
Tatu: watu
hawa ni lazima wawe na uelewa, na uelewa huu haijalishi na kuhusiana na nini,
inaweza kuwa jinsi wao wenyewe wanavyoishi, au inaweza kuwa ni uelewa juu ya
watu waliokuwa kabla yao, Cha muhimu ni kwamba watu hawa wana uelewa.
Na hapa
ndipo tunafikia katika hatua ya kusema kwamba neno "tamaduni” maana yake ni:
mkusanyiko wa watu fulani wanaoishi katika mazingira fulani wakiwa na uelewa wa
kila jambo wanalolisimamia. Na kwa maana hii tunakuwa tumefikia hatua fulani
katika kuelezea maana ya tamaduni na pia kuweza kutambua kwamba neno hili
hutumika mahala gani.
Itaendelea.....